Sunday, May 27, 2012

SITA WAHOJIWA SINGIDA KWA TUHUMA ZA UBADHIRIFU WA ZAIDI YA SH. MILIONI 80.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida SSP Ayoub John Tenge akitoa taarifa kwa mwandishi wa habari wa MO BLOG (hayupo pichani) juu ya kuhojiwa kwa wafanyakazi wa manispaa ya Singida kwa tuhuma ya ubadhirifu wa shilingi milioni 86. Fedha hizo zimedaiwa kuwa ni za malipo ya madai mbalimbali ya walimu wa shule za msingi na Sekondari.

Jengo la makao makuu ya halmashauri ya manispaa ya Singida. (Picha zote na Nathaniel Limu).
Na.Nathaniel Limu.
Wafanyakazi wanne wa halmashauri ya manispaa ya Singida akiwemo mkaguzi wa ndani Andrew Masanja wamehojiwa na polisi kwa tuhuma ya ubadhirifu wa shilingi 86 milioni.
Fedha hizo zilizotoka hazina nyingi zinadaiwa zilikuwa ni malipo mbalimbali ya madai ya walimu wa shule za msingi na sekondari.
Wafanyakazi hao ambao walihojiwa kati ya wiki hii ni kutoka idara ya elimu, uhasibu na ofisi ya mkaguzi wa ndani.
Habari za uhakika kutoka ndani ya jeshi la polisi mjini Singida, zinadai fedha hizo zimetafunwa kati ya Januari na Machi mwaka huu.
Kaimu Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Singida SSP Ayoub John Tenge, alikiri ofisi yake kuwahoji wafanyakazi hao na kwamba bado wanaendelea kuwahoji zaidi na idadi yao inategemewa kuongezeka.
Tenge amesema kwa sasa hayupo tayari kufafanua zaidi au kutaja majina ya watuhumiwa na wale ambao wanatarajia kuwahoji kwa madai kuwa kitendo hicho kinaweza kuvuruga upelelezi.
Kaimu Kamanda huyo amesema mambo yakiiva, atatangaza hadharani majina ya watuhumiwa ili jamii iweze kujua kilichofanyika kwenye manispaa yao.

HABARI NA, MO BLOG
 


No comments:

Post a Comment